Kocha Mkuu wa mabingwa watetezi wa Ligi Kuu ya Vodacom, Mbelgiji Patrick Aussems, amesema ataendelea kuwanoa washambuliaji wake ili waweze kufunga mabao mengi zaidi katika mechi zinazofuata
Aussems ambaye tayari timu yake imefunga mabao matano msimu huu, amesema anahitaji kuona safu yake ya ushambuliaji inatumia vema nafasi za kufunga wanazozitengeneza na hatimaye kupata ushindi mnono katika kila mechi watakayocheza.
Aussems alisema kila mechi ya Ligi Kuu Tanzania Bara ni ngumu, na ili kujiweka katika nafasi salama zaidi ni kupata mabao mengi ambayo yatawahakikishia kuondoka na pointi tatu.
"Nawapongeza kwa kucheza vizuri na kupata ushindi katika mechi mbili tulizocheza za Ligi Kuu, lakini bado hawatumii vizuri nafasi ambazo wametengeneza, katika mechi dhidi ya Mtibwa Sugar, wamepoteza nafasi kama tatu nyingine za kufunga, tunahitaji kulimaliza tatizo hili," Aussems amenukuliwa na Nipashe
Aliongeza kuwa anahitaji kuona hawarudii makosa katika mechi ijayo dhidi ya Lipuli Fc na kupata ushindi ili kuendelea kukaa kileleni katika msimamo wa ligi hiyo inayoshirikisha timu 20 kutoka sehemu mbalimbali hapa nchini.
Naye nahodha msaidizi wa timu hiyo, Mohammed Hussein "Zimbwe Jr" amesema kikosi chao kina kiu ya kutwaa ubingwa wa ligi hiyo kwa msimu mwingine wa tatu mfululizo.
"Tunajua hakuna mechi rahisi, timu zote zimejiandaa kuonyesha ushindani, kila mchezo kwetu tunauona kama fainali, naamini tutaendelea kupambana ili tutimize malengo yetu, tunaomba ushirikiano uliokuwapo, uendelee," Zimbwe Jr alisema.
Simba inaongoza ligi ikiwa na pointi sita baada ya kupata ushindi wa mabao 3-1 dhidi ya JKT Tanzania na Ijumaa ilipata ushindi wa mabao 2-1 walipoikaribisha Mtibwa Sugar kutoka Manungu, Turiani mkoani Morogoro

No comments:
Post a Comment