Mwenyekiti wa Yanga Dk Mshindo Msolla amesema timu hiyo inakamilisha usajili wa mlinda lango wa Bandari Fc Farouq Shikalo ili kuwa na idadi ya nyota nane wapya wa kigeni ambao wataitumikia timu hiyo msimu ujao
Aidha Dk Msolla amesema nyota hao wataungana na Wacongomani Klaus Kindoki na Papi Tshishimbi aliyeongeza mkataba wa miaka miwili
Kauli hiyo ya Dk Msolla inamaliza tetesi za kuachwa kwa mlinda lango Kindoki ambaye alikuwa kwenye hatihati ya 'kukatwa'
"Kabla mwalimu hajaondoka alionesha mahitaji yake, tulikaa naye kwa muda mrefu na mahitaji yake aliyoainisha kwanza aligawa wachezaji katika makundi manne," amesema Dk Msolla
"Wachezaji wa nje aliowahitaji ni Issa Bigirimana, Papy Sibomana, Juma Balinya na kuna mwingine anatoka Namibia na Kalengo"
"Kwa hiyo wote wanaocheza mbele aliowahitaji tumewapata lakini nafasi ya ulinzi alimuhitaji Lamine na nahodha wa timu ya taifa ya Burundi anaitwa Yusufu ambao nao tumewapata."
"Sasa hivi tunahangaika na mchezaji mmoja ambaye ni golikipa wa timu ya Bandari ya Kenya ambaye yupo Misri na timu yake ya taifa"
"Mchakato unaendelea vizuri na walikutana wakati timu zao zikiwa Hispania kwa maandalizi ya AFCON kwa hiyo tupo kwenye hatua za mwisho kwenye hilo"
"Maana yake tukimpata golikipa wa Kenya tutakuwa na wachezaji 8 wa kimataifa na mwalimu ametaka waliokuwepo wabaki wawili Kindoki na Tshishimbi"
"Wengine wote wamemaliza mikataba yao kwa hiyo wataondoka salama kama wanamadai basi ni ya kawaida tu ambayo ni mishahara na bonasi zao"
Kwa hivyo kiungo Thabani Kamusoko na mshambuliaji Amissi Tambwe wanaungana na Heritier Makambo kuwa wachezaji wa kigeni ambao hawatakuwa sehemu ya kikosi cha Yanga msimu ujao

No comments:
Post a Comment